Hotuba ya Baba Mtakatifu Fransisko kwa wawakilishi wa Njia ya Neokatekumenato, 1-2-2014

Hotuba ya Baba Mtakatifu Fransisko kwa wawakilishi wa Njia ya Neokatekumenato, 1-2-2014

Fransisko

Ndugu wapendwa:

Namshukuru Bwana kwa furaha ya imani yenu na kwa bidii ya ushuhuda wenu wa kikristo, shukrani kwa Mungu! Nawasalimu wote kwa moyo mkunjufu, nikianza na kikundi cha kimataifa cha wajibikaji wa Njia ya Neokatekumenato, pamoja na mapadre, waseminari na makatekista. Ninatuma salamu iliyojaa upendo kwa watoto, mliopo hapa kwa wingi. Mawazo yangu yanaelekea hasa kwa familia, ambazo zitaenda kwenye sehemu mbalimbali za dunia kutangaza na kushuhudia Injili. Kanisa linawashukuru kwa ukarimu wenu. Ninawashukuru kwa yote mnayofanya katika Kanisa na duniani.

Na haswa kwa jina la Kanisa, Mama yetu—Mama yetu Kanisa Takatifu, lenye mpangilio kingazi, kama alivyopenda kusema mtakatifu Inyasi wa Loyola—, kwa jina la Kanisa ningependa kushauri baadhi ya mapendekezo rahisi. La kwanza ni kuwa na uangalifu mkubwa wa kujenga na kuhifadhi ushirika ndani ya Makanisa mahalia ambapo mtakwenda kufanya kazi. Njia ina karama yake yenyewe, elimumwendo yake yenyewe, kipaji ambacho, kama karama zote za Roho, mandhari yenye kina ya kikanisa; maana yake ni kusikiliza maisha ya Makanisa ambapo wawajibikaji wenu wanawatuma, kuthaminini hazina zao, kuteseka kwa madhaifu ikiwa inabidi na kutembea pamoja kama kundi moja, chini ya uongozi wa Wachungaji wa Makanisa mahalia. Ushirika ni wa msingi: wakati mwingine inaweza kuwa bora kujikana kuishi kwa namna zote ambazo utaratibu wenu ungehitaji ili kudhamini umoja kati ya ndugu walio ndani ya ile jumuiya moja ya kikanisa, ambayo daima mnapaswa kujisikia sehemu yake.

Pendekezo lingine: popote mtakapoenda, itawasaidia kukifikiri kwamba Roho wa Mungu daima anafika kabla yetu. Hiyo ni muhimu: Bwana daima anatutangulia! Mfikireni Filipo, wakati Bwana anamtuma njiani ambapo anakutana na mtendaji akiketi katika gari lake (taz. Mdo. 8, 27-28). Roho alifika wa kwanza: alikuwa akimsoma nabii Isaya bali hakuelewa, lakini moyo wake uliwaka. Hivyo, Filipo anapomkaribia, yeye ameshatayarishwa kwa ajili ya katekesi na Ubatizo. Roho daima hutangulia. Mungu daima anafika kabla yetu! Hata katika sehemu za mbali zaidi, pia katika tamaduni zilizo tofauti zaidi, Mungu hueneza katika kila mahali mbegu za Neno lake. Kutoka hapa inazalishwa haja ya umakini maalum kwa mazingira ya kitamaduni ambapo ninyi, familia, mtaenda kufanya kazi: ni mazingira ambayo mara nyingi ni tofauti sana na yale mnayotoka. Wengi wenu mtajitahidi kujifunza lugha mahalia ambayo pengine ni ngumu, na hiyo juhudi inathaminiwa. Muhimu zaidi sana itakuwa juhudi yenu ya “kujifunza” tamaduni mtakazokutana nazo, mkijua kutambua uhitaji mahalia wa Injili lakini vile vile upo utendaji ambao Roho Mtakatifu ametekeleza katika maisha na historia ya kila jamii.

Na hatimaye, nawasihi mjaliane kwa upendo, kwa namna ya pekee kwa walio wadhaifu zaidi.

Familia wapendwa, ndugu wapendwa, ninawapa moyo kupeleka Injili ya Yesu Kristo kila mahali, hata katika mazingira yaliyopoteza zaidi Ukristo wao, hasa kwa wale watu waliowekwa pembeni zaidi . Mwinjilishe kwa upendo, wapelekeeni wote upendo wa Mungu. Waambieni wale mtakaokutana nao kwenye njia za utume wenu kwamba Mungu anampenda mwanadamu jinsi alivyo, pamoja na mipaka yake, na makosa yake, na pia na dhambi zake. Ndiyo maana alimtuma Mwanae, ili Yeye achukue dhambi zetu juu yake mwenyewe. Iweni wajumbe na mashahidi wa wema usio na mipaka na wa huruma isiyomalizika ya Baba.

Ninawakabidhi kwa Mama yetu, Maria, ili avuvie na kutegemeza utume wenu. Katika shule ya Mama huyu mwororo, muwe wamisionari wenye ari na furaha. Msiipoteze furaha, songeni mbele!